Eneo la Kiambu Road limeelezwa kuwa jiji jipya la kijani. Eneo hili jipya la ‘dhahabu’ liko karibu na mji wa Nairobi, na hii imefanya kuwa kivutio kwa wakazi wa Nairobi wanaotafuta maisha bora.
Kwa kweli, Wakenya wengi walio na pesa mpya wanajitokeza hapa. Wengi wao wanataka kujionjia maisha bora – mbali na kelele ambazo mara nyingi zimekuwa zikihusishwa na Nairobi.
Familia changa zinazotafuta mazingira tulivu, yenye hali ya nyumbani mbali na kelele za jiji na hewa iliyojaa uchafu pia zimejiunga na mchakato huu.
Wanaume na wanawake wasio na familia wanaipenda pia.
Miaka michache iliyopita, ardhi ilikuwa ni mashamba makubwa ya chai – na vijiji. Leo – ardhi hiyo imejaa nyumba za kisasa; nyumba nzuri ambazo zinazidi kuwa kivutio miongoni mwa tabaka la kati, hata kwa vijana wanaoanza kazi zao za kwanza.
Kwa mujibu wa wakazi wa hapa, eneo lina huduma za jamii zinazotosha; hospitali, shule nzuri, maeneo ya ununuzi, viwanja vya watoto, na mazingira mazuri.
“Ninapenda hapa kwa sababu ni baridi na hewa ni safi. Barabara ni nzuri, na hapa ni salama,” alisema Maryanne Mwangi alipozungumza na Wananchi Reporting.
Anasema kwamba eneo hili limeona ukuaji wa kasi huku watu wengi, hasa wale walio na familia ndogo na wanaoanza kukua katika maisha yao ya kazi, wakipenda eneo hili.
“Hakuna majengo marefu sana hapa, ni ya asili na mtu anaweza kufurahia matembezi ya jioni huku akifurahia hali ya kijiji,” aliongeza.
Wakazi wengi wa asili, wamiliki wa zamani wa ardhi, wameshauza ardhi yao na kuhamia sehemu za ndani – huku mji wa Nairobi ukiendelea kupanuka.
Jane, mtaalamu wa mawasiliano Nairobi alisema kwa Wananchi Reporting kwamba alihamia Kiambu Road zaidi ya mwaka mmoja uliopita.
“Niliishi kando ya Mombasa Road, lakini hivi karibuni niliamua kuhamia hapa. Ninapenda mazingira, na ukweli kwamba nasikia ndege wakiteta asubuhi. Hapa ni tulivu sana, na kuna hali ya nyumbani,” alisema.
Wengi wanasema kwamba eneo hili bado halijageuka kuwa jiji la mawe kama ilivyo katika maeneo kama Kileleshwa.
Ekari moja katika sehemu za mapema za Kiambu Road inaweza kugharimu hadi Ksh.80 Milioni. Robo ya ekari inagharimu kati ya Ksh.15 na 20 Milioni.
Kodi ya pango – ni ya juu – ambapo nyumba ya chumba kimoja inaweza kugharimu hadi Ksh.25,000 kwa mwezi. Unit yenye vyumba viwili vya kulala huanza kutoka Ksh.45,000 kwa mwezi. Unit yenye vyumba vitatu na nne inagharimu kati ya Ksh.65,000 na Ksh.145,000 kwa mwezi. Hata hivyo, gharama hizi hazijazuia ‘hamahama kubwa’.